“Maelezo yameibuka kuhusu jinsi moto mbaya ulioteketeza bweni katika shule ya Utumishi Girls Senior Secondary School huko Gilgil, Kaunti ya Nakuru, ulivyoripotiwa kwa mara ya kwanza kwa polisi alfajiri ya Alhamisi. Kulingana na ripoti ya polisi iliyowasilishwa katika Kituo cha Polisi cha Gilgil, tukio hilo liliripotiwa rasmi saa 10:30 alfajiri na mkuu wa shule hiyo, Bi Joycelene Muraguri, baada ya moto kuzuka katika moja ya mabweni ya shule hiyo. Ripoti hiyo inaonyesha kuwa Bi Muraguri aliwaarifu maafisa kuhusu mlipuko huo wa moto, hatua iliyosababisha hatua za haraka zilizowahusisha polisi, maafisa wa upelelezi, wazima moto na vikosi vya uokoaji. Baada ya taarifa hiyo, Kamanda wa Polisi wa Kaunti Ndogo ya Gilgil (SCPC) aliongoza maafisa kutoka kituo cha polisi pamoja na wachunguzi kutoka Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) hadi shuleni humo iliyoko takriban kilomita saba kaskazini mwa mji wa Gilgil. Maafisa walipowasili eneo la tukio, walikuta bweni lijulikanalo kama Meline Waithera tayari likiwa limeteketezwa na moto. Polisi walisema bweni hilo lilikuwa na takriban wanafunzi 220 kutoka Gredi 10, Kidato cha Tatu na Kidato cha Nne. Vikosi vya dharura kutoka mashirika mbalimbali vilitumwa kudhibiti moto huo huku taharuki ikienea ndani ya shule. Magari ya zimamoto kutoka Naivasha, Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF), Huduma ya Misitu Kenya (KFS), Huduma ya Kitaifa kwa Vijana (NYS) yaliungana kupambana na moto huo. Ripoti ya polisi inaeleza kuwa juhudi za pamoja za mashirika hayo zilifanikiwa kuudhibiti moto huo kabla haujasambaa katika sehemu nyingine za shule. Hata hivyo, tukio hilo lilisababisha uharibifu mkubwa pamoja na vifo vya wanafunzi kadhaa. Mamlaka zilikadiria idadi ya waliofariki kuwa 16 ingawa maafisa walisema huenda idadi hiyo ikabadilika huku uchunguzi na kutambua miili kukiendelea. Idadi isiyojulikana ya wanafunzi waliojeruhiwa na kupata mshtuko walipelekwa katika hospitali za karibu kwa matibabu. Wanafunzi waliojeruhiwa walipelekwa katika Hospitali ya Kaunti Ndogo ya Gilgil pamoja na Hospitali ya St Mark’s ambako walilazwa wakiwa katika hali tulivu. Maafisa wa Kitengo cha Uchunguzi wa Maeneo ya Uhalifu (CSI) kutoka Nakuru waliwasili eneo la tukio huku wachunguzi wakianza uchunguzi kuhusu chanzo cha moto huo. Mamlaka zilisema chanzo cha moto huo bado hakijajulikana. Mkasa huo ni wa hivi punde katika msururu wa visa vya moto katika shule mbalimbali nchini katika miaka ya karibuni, hali inayozua upya wasiwasi kuhusu viwango vya usalama katika shule za bweni.
Original story
Continue reading at Taifa Leo (Swahili)
taifaleo.nation.co.ke
Summary generated from the RSS feed of Taifa Leo (Swahili). All article rights belong to the original publisher. Click through to read the full piece on taifaleo.nation.co.ke.
