“SEKTA ya kibinafsi, benki na wahasibu wametaka Bunge kupunguza kiwango cha juu cha ushuru wa Kulipa kulingana na Mapato (PAYE) kutoka asilimia 35 hadi asilimia 30 kwa wafanyakazi wote wanaolipa ushuru wa mishahara. Wadau hao waliambia Kamati ya Bunge ya Fedha na Mipango ya Kitaifa kuwa hatua hiyo itaongeza mapato ya serikali kwa takriban Sh28.1 bilioni na kusaidia kuunda nafasi 36,000 za kazi kila mwaka. Muungano wa Sekta ya Kibinafsi Kenya (Kepsa), uliwasilisha mapendekezo yake mbele ya kamati hiyo ukitaka ifanye marekebisho katika Mswada wa Fedha wa 2026 ili kupunguza kiwango cha ushuru katika viwango vyote vitano vya PAYE. Mwenyekiti wa Kepsa, Jaswinder Bedi, alisema mfumo wa sasa una viwango vitano vya ushuru ambapo kiwango cha juu zaidi ni asilimia 35 kwa mapato ya zaidi ya Sh9.6 milioni kwa mwaka au Sh800,000 kwa mwezi. “Kepsa inapendekeza marekebisho katika Jedwali la Tatu la Sheria ya Ushuru wa Mapato ili kiwango cha juu cha PAYE kisizidi asilimia 30,” alisema. Mapendekezo hayo yanaonyesha kuwa asilimia 10 itatozwa kwa Sh30,000 za kwanza, asilimia 20 kwa kiwango kinachofuata, asilimia 25 kwa mapato yanayofuata, asilimia 27.5 kwa kiwango kingine na asilimia 30 kwa mapato yanayozidi Sh800,000. Aidha, Kepsa imependekeza kiwango cha msamaha wa ushuru wa kibinafsi kiongezwe hadi Sh3,000 kwa mwezi na mapato yasiyotozwa ushuru yawe Sh30,000. Dkt Bedi alisema wafanyakazi wengi wameathiriwa vibaya na kupanda kwa gharama ya maisha pamoja na ushuru mpya kama ule wa nyumba nafuu wa asilimia 1.5 na mchango wa asilimia 2.75 kwa Hazina ya Bima ya Afya ya Jamii (SHIF). Alisema kiwango cha ushuru wa asilimia 35 kwa wafanyakazi ni kikubwa kuliko ushuru wa asilimia 30 unaotozwa kampuni kwa faida zao. “Kupunguza ushuru huu kutarejesha Sh28.1 bilioni kwa wafanyakazi, kuongeza matumizi ya nyumbani, kupunguza mikopo na kukuza uchumi kwa Sh210 bilioni ndani ya mwaka mmoja,” alisema. Mkurugenzi Mkuu wa Chama cha Benki Kenya (KBA) Raimond Molenje, alisema iwapo PAYE itapunguzwa kwa asilimia tano, benki zitaweza kutoa mikopo ya hadi Sh10 bilioni zaidi kwa wananchi kutokana na kuongezeka kwa mapato ya matumizi. Kwa upande wake, mshirika wa masuala ya ushuru katika Grant Thornton Samuel Mwaura, alisema wafanyakazi wa sekta rasmi tayari hulipa ushuru kikamilifu bila nafasi ya kukwepa kodi, hivyo wanabeba mzigo mkubwa wa ushuru kuliko sekta isiyo rasmi. “Kuongeza mishahara inayobaki mikononi mwa wafanyakazi kutachochea matumizi ya bidhaa za nyumbani na kuongeza mapato ya VAT na ushuru mwingine,” alisema. Bw Mwaura pia alipinga pendekezo la kuwatoza ushuru wafanyakazi wa kandarasi za muda mfupi kwenye malipo yao ya mwisho, akisema hatua hiyo itaathiri wafanyakazi wa mashirika yasiyo ya serikali, sekta ya ujenzi na miradi ya muda. Wadau hao pia walitaka kufutwa kwa mapendekezo ya kuongeza ushuru kwa miamala ya kidijitali, malipo ya kadi, huduma za kifedha za kidijitali pamoja na sheria mpya za kutoa taarifa za kifedha. Dkt Bedi alisema mfumo bora wa ushuru unapaswa kuhimiza uwekezaji, kuongeza nafasi za kazi na kupanua msingi wa walipa ushuru badala ya kuongeza ushuru kwa kundi dogo la wafanyakazi rasmi. Alisema Kenya inapaswa kuoanisha sera zake za ushuru na zile za Jumuiya ya Afrika Mashariki ili kubaki kitovu kikuu cha biashara na uwekezaji katika eneo hili.
Original story
Continue reading at Taifa Leo (Swahili)
taifaleo.nation.co.ke
Summary generated from the RSS feed of Taifa Leo (Swahili). All article rights belong to the original publisher. Click through to read the full piece on taifaleo.nation.co.ke.
